Kwa nini utaendelea kuishiwa pesa
hata kama unaingiza kipato (sehemu ya pili) – Dr Lawi Mshana
Watu wengi hawaishiwi pesa kwa sababu ya umasikini bali
kushindwa kusimamia fedha zao. Kwa hiyo hata wenye uwezo mzuri kifedha wamekuwa
wakiishiwa fedha pia. Lazima tujiulize kwanini hata wenye kipato kizuri
wanaishiwa pesa.
NB: Katika makala iliyopita nilizungumzia kipengele namba 1
hadi 10.
11. Unatumia
pesa nyingi kuliko unazoingiza
Chanzo kikuu
cha kufilisika kwa wengi ni kutumia pesa nyingi kuliko pesa anazoingiza. La
kufanya hapa ni kupunguza (kubana) matumizi na kuongeza kipato zaidi.Ukipitia
vizuri matumizi yako utagundua kwamba kuna matumizi ungeweza kuyaepuka kwa muda
na bado ukaweza kuishi. Lakini pia ungeweza
kugundua kwamba zipo njia ambazo zinaweza kukuingizia kipato ingawa hujawahi
kuzifanya. La msingi ni kutoka katika maisha ya mazoea unayoyafurahia hata kama
hayana msaada kwako (comfort zone).
12. Unawekeza
kwenye vitu badala ya kwako mwenyewe
Pengine
unanunua vitu vya anasa ambavyo sio vya kiwango chako cha maisha au umepanga
kwenye nyumba ambayo sio ya kiwango chako cha maisha. Badala yake ungewekeza
zaidi kwenye elimu yako, uwekezaji wa maana na kuweka akiba. Ni aibu kununua
vitu vya kifahari lakini hujiwekei akiba wala hujiungi na mfuko wa hifadhi ya
jamii.
13. Unajaribu
kuwa tajiri kwa haraka
Watu wengi
wanatafuta njia ya kuondokana na umasikini kwa kutafuta utajiri wa haraka. Wako
tayari kuwekeza zaidi kwenye bahati nasibu na kuhatarisha maisha yao kwa wizi
au rushwa kuliko kuwekeza kwenye shughuli zinazoeleweka na kukubalika.
Ukifuatilia matajiri wengi utagundua kwamba hawakutajirika kwa siku moja. Mara
nyingi tunajikita katika kuangalia mafanikio yao ya leo na kusahau kufuatilia
historia ya nyuma kabla ya utajiri wao.
14. Huzingatii
bajeti yako
Watu wengi
sio tu kwamba hawazingatii bajeti yao bali hata bajeti yenyewe hawana.
Unapokosa bajeti pesa zako zinakuwa na walaji wengi wasio rasmi. Uwe masikini
au tajiri unahitaji sana bajeti ili ugundue matatizo yako ya kifedha na kuboresha
hali yako ya kifedha.
15. Huna
mpango wa maisha
Unaishi kwa
kutegemea dharura zaidi kwa vile huna mpango wa maisha yako. Vitu vingi
unavyogharamia ni vya kushtukiza badala ya mpango kamili. Huwezi kusimamia
jambo litokee kwa vile huna mpango thabiti wa maisha. Ukishindwa kupanga,
umepanga kushindwa!
16. Unanunua
vitu vinavyoshuka thamani
Sababu
mojawapo ya watu kuwa masikini ni kununua zaidi vitu vinavyoshuka thamani kama
magari, mitumbwi nk. Hali hii inawafanya watu kuwa na raslimali chache za
kujenga utajiri na kujikuta wanaishi kwa kutegemea mshahara peke yake. Inafaa
kununua zaidi vitu vinavyoongezeka thamani kv ardhi, hisa na biashara ya
mtandao.
17. Huko
tayari kujitoa kisadaka
Watu wengi
wanadhani mafanikio yatakuja kwa kuwa na ujuzi peke yake. Ni asilimia 20 tu ya
ujuzi wa kichwani inahitajika kwa ajili ya mafanikio. Sehemu kubwa inahitaji
kubadilika kivitendo na kimtazamo ili tufanikiwe. Na wengi hawako tayari
kuhatarisha maisha yao kwa ajili ya mafanikio.
18. Unajaribu
kufanya mambo mengi kwa mara moja
Wengi
wanakuwa masikini kwa sababu ya uroho wa kutaka kila kitu kwa kipindi kifupi.
Unapoamua upate kila unachohitaji kwa mara moja lazima ukwame. Weka vipaumbele
vya maisha yako vinavyoendana na raslimali zilizopo. Hutafanikiwa kwa kuamua kulipia
masomo ya gharama kubwa na kujenga nyumba wakati huohuo. Fanya jambo moja baada
ya jingine.
19. Unalipa
kiasi kikubwa kwa ajili ya simu yako ya mkononi
Kuna watu
wamenunua simu za bei mbaya wakati wanazitumia kwa matumizi sawa na ya simu
ndogo. Mwingine hata internet hajui lakini ana simu ya bei mbaya ili
kuringishia watu. Lakini pia kuna watu wanagharamia mawasiliano kwa simu kuliko
chakula wanachokula. Na kibaya zaidi simu hizo hazichangii chochote katika
maisha yao ya kiuchumi.
20. Hutaki
kuongeza ujuzi wala mafunzo
Unaporidhika
na kiwango chako cha elimu hata pale fursa za kusoma zinapopatikana, unaendelea
kubaki na kiwango chako cha kipato kwa kipindi kirefu. Kadiri unavyoongeza
elimu ndivyo, unavyojiweka katika nafasi ya kupata kazi ya maana zaidi na yenye
kipato zaidi. Hata hivyo mafunzo si kwa ajili ya ajira peke yake. Unaweza kuwa
umeajiriwa na ukaongeza ujuzi wa ufugaji, kilimo, biashara ya mtandao nk.
0 Comments
Karibu sana na ujisikie huru kushirikisha mawazo yako au kuuliza swali tujifunze pamoja (Welcome and feel free to share your thoughts or ask questions so we can learn together)