Ticker

6/recent/ticker-posts

Kwanini utaendelea kuishiwa pesa hata kama unaingiza kipato? (sehemu ya kwanza)

Kwa nini utaendelea kuishiwa pesa hata kama unaingiza kipato (sehemu ya kwanza) – Dr Lawi Mshana

Watu wengi hawaishiwi pesa kwa sababu ya umasikini bali kushindwa kusimamia fedha zao. Kwa hiyo hata wenye uwezo mzuri kifedha wamekuwa wakiishiwa fedha pia. Lazima tujiulize kwanini hata wenye kipato kizuri wanaishiwa pesa.

1. Kufanya maamuzi ya kukurupuka

 Unapokuwa kwenye msongo wa mambo fulani ni rahisi kufanya maamuzi ya kukurupuka na kujikuta ukiishiwa pesa. Ndiyo maana hata mtu anayetaka kununua vitu madukani anashauriwa afanye ‘window shopping’ (aende kujua bei akiwa hana pesa mfukoni) ndipo siku nyingine aende na pesa kwa ajili ya kufanya manunuzi. Bila hivyo atajikuta akinunua kitu asichohitaji au kwa bei kubwa na baadaye kukikuta duka jingine kinauzwa kwa nusu ya bei aliyonunulia. 

2. Unapuuzia madeni makubwa

Watu wengi hawana mkakati wowote wa kulipa au kupunguza madeni makubwa. Lazima ujifunze kushughulikia madeni makubwa uliyo nayo kama unavyoshughulikia madogo. Ukiyapuuzia unafikia mahali unatumia pesa zako kana kwamba hudaiwi na siku utakapofuatiliwa utakuwa na hali mbaya sana kifedha. Unapopunguza deni kubwa unaweza kumvutia anayekudai kukusamehe kabla hujalimaliza. Huwezi kueleweka kama unaendelea vizuri na maisha bila kupunguza kabisa deni la watu.

3. Unajidharau na kujiona mnyonge

Mtu akiwa na ugumu wa kifedha halafu akajidharau, hatafanya chochote ili kuibadilisha hali yake. Lazima tujue kwamba kuna kazi nyingi mpya ambazo tunaweza kujifunza leo ambazo zinaweza kubadilisha maisha yetu. Tuache mazoea ya kufanya kazi zilizofanywa wakati wa mkoloni ambazo hazitatui changamoto za watu wa leo. Inasemekana wengi wetu hatutumii 10% ya uwezo tuliopewa na Mungu katika ubongo wetu. Tungeliweza kufanya makubwa ila hatutumii akili zetu ipasavyo.

4. Hujajifunza kudhibiti fedha zako binafsi

Kuna watu wanakopa bila hata kujua vizuri riba au jinsi watakavyokatwa na muda wa makato hayo. Matokeo yake mtu analipia deni takriban mara mbili ya pesa alizokopeshwa. Na kibaya zaidi amekopa kwa ajili ya kufanya kitu ambacho hakikuwa na uharaka kiasi hicho. Au anajikuta mkopo huo hautoshi hiyo shughuli yake hivyo anaongeza mkopo mwingine juu yake. Usikope pesa ili UJIFURAHISHE bali UPATE UHURU WA KIFEDHA katika siku zijazo. Ni kosa kubwa kukopa mkopo wa riba kwa ajili ya kununua vitu ambavyo havikuingizii wala kuchangia chochote katika maisha yako.

5. Hujilipi kwanza 

Unakuwa masikini kwa vile hujilipi wewe mwenyewe kwanza. Kujilipa mwenyewe ni kuweka kiasi fulani kama akiba kabla ya kutumia kilichobaki kwa ajili ya matumizi. Kila unapopata pesa unawaza tu matumizi lakini kamwe huwazi kuhusu akiba. Kuna mtu aliwahi kusema hapati pesa zinazotosha kuweka akiba. Lakini mtu huyohuyo ukimfuatilia sana anachangia sherehe kadhaa kwa mwezi, anahonga wanawake na kununua vinywaji ambavyo vinadhoofisha kinga ya mwili wake.

6. Unatanguliza furaha ya leo kabla ya mahitaji ya kifedha ya baadaye (siku zijazo)  

Unawaza zaidi jinsi utakavyojifurahisha kwa kutumia pesa zako leo bila kufikiri kuhusu maisha yako ya baadaye. Jiulize vitu unavyonunua leo kiasi gani vitakusaidia katika maisha yako ya miaka ya mbeleni. Lazima uanze kujiuliza nguvu zikipungua au kazi yako ikifikia mwisho itakuwaje ndipo utaona umuhimu wa kuandaa maisha ya baadaye. Badala ya kununua vipodozi vingi leo utaanza kuvipunguza ili uandae maisha yajayo.

7. Huna mfuko wa dharura

Huu mfuko wa dharura ni wa kukusaidia ukipata dharura za maisha, ukiwa mzee (ukistaafu) au ukiondoka duniani (unawaachaje waliobaki). Kwa hiyo hata kama utakuwa huwezi kufanya kazi unazozifanya leo mfuko huu utakusaidia. Vinginevyo kiwango chako cha maisha kinaweza kushuka ghafla. Mfuko huu sio lazima uutunze wewe mwenyewe. Ziko taasisi za mifuko ya hifadhi za jamii ambazo ziko kwa ajili hiyo.

8. Una matumizi makubwa sana kwenye gharama ya nyumba

Pengine unatumia pesa nyingi sana kwenye kulipia deni la nyumba au kodi kubwa. Inashauriwa utumie kiasi kisichozidi 20% ya kipato chako kwenye gharama za nyumba. Huna haja ya kung’ang’ania mjini ikiwa unalipa gharama kubwa ya nyumba. Na huna sababu ya kukopa kwa ajili ya nyumba kubwa sana isiyoendana na uwezo wako kifedha.

9. Hujui pesa yako inakwenda wapi

Unaishiwa kwa vile huna bajeti. Kama hujui pesa yako inakwenda wapi, huwezi kuigeuza ielekee ule upande ambao utakuwa na manufaa kwako. Unapojua kwamba una pesa za kutosha kushughulikia mahitaji yako yote na baadhi ya mambo ambayo sio ya lazima sana, unalala usingizi mzuri usiku. Kama hujui pesa zako zinakwenda wapi, hata kama kipato kitaongezeka hakuna mabadiliko yatakayotokea kwenye maisha yako.    

10. Hutofautishi matamanio (wants) na mahitaji (needs)

Kwa ujumla watu wanapata shida sana kutofautisha matamanio na mahitaji. Wanatumia neno ‘mahitaji’ takriban kwa kila kitu wanachonunua wakidhani wanapaswa kufanya hivyo. Unaweza KUHITAJI gari kwa ajili ya usafiri au KUTAKA/KUTAMANI gari la kifahari ili nawe uonekane tajiri. Mtazamo huu umeshusha wengi kiuchumi. Tambua unahitaji nini (needs) na unataka nini (wants).

…..Somo hili litaendelea siku nyingine


Post a Comment

0 Comments